Alhamisi, 2 Novemba 2017

RC : Wawekezaji Shirikianeni na Serikali

KAIMU Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Ayoub Mohammed Mahamoud, amesema lengo la serikali ni kuhakikisha sekta ya utalii inaimarika na kuleta tija kwa nchi na wananchi wake.

Ayoub ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa Mjini Magharibi, alieleza hayo kwenye mkutano uliowakutanisha uongozi wa mkoa huo na wawekezaji wa sekta ya utalii katika mkoa huo.

Ayoub aliwataka wawekezaji hao kuendelea kushirikiana na serikali ambayo ina nia ya dhati ya kuzipatia ufumbuzi changamoto hizo sambamba na kushirikiana na wananchi kwenye maeneo ya uwekezaji.

Alisema serikali itaendelea kutimiza wajibu wake wa kuweka mazingira mazuri katika sekta ya utalii, lakini pia na wawekezaji wana haki ya kutekeleza majukumu yao katika kuchangia kukuza sekta hiyo.

Katika hatua nyengine mkuu huyo aliagiza kutiwa ndani kwa kosa la utovu wa nidhamu meneja wa shirika la Umeme (ZECO) Kanda ya kaskazini Khamis Mbarouk Kitwana kwa kukaidi wito wa kutakiwa kushiriki katika mkutano huo.

Mkuu huyo alimuita meneja huyo kwa ajili kutoa maelezo juu ya tatizo la kukatika mara kwa mara kwa umeme katika maeneo ya hoteli za kitalii katika eneo hilo.

Kwa upande wao wawekezaji hao wa hoteli za kitalii  walisema kutoimarishwa kwa miundombinu ya barabara, umeme, maji safi na salama kwenye maeneo ya hoteli ni mongoni mwa mambo yanayoongeza gharama za uendeshaji kwenye miradi yao.

Wakizungumza katika kikao cha pamoja na uongozi wa mkoa wa Kaskazini Unguja katika ukumbi wa ofisi ya mkoa huo, huko Mkokotoni wamesema kuwa matatizo hayo kwa kiasi kikubwa yamekuwa yakirudisha nyuma maendeleo ya sekta hiyo.

Katika kikao hicho, wawekezaji hao waliiomba serikali kuhakikisha inazifanyia kazi changamoto hizo za miundombinu ya kijamii ili mizgo wa gharama za uendeshaji uweze kupungua.

Sorce Zanzibar leo